DIAMOND MATATANI ARUSHA AHUSISHWA NA UTAPELI,WACHEZA SHOO WAKE WATIWA MBARONI





Na Woinde Shizza 
wa Globu ya Jamii, Arusha


JESHI la polisi mkoni Arusha, linamsaka msanii nguli wa kizazi kipya wa jijini Dar es salaam,Nasibu Abdul Juma almaarufu kama Diamond (pichani) kwa tuhuma za utapeli wa kujipatia kiasi cha shilingi milioni 1.5 na kushindwa kuhudhuria shoo jijini Arusha na kusababisha vurugu  na uharibifu mkubwa wa mali katika ukumbi maarufu wa Triple A.


Diamond anadaiwa kuingia mkataba na kampuni ya Arbab Mb Entertaiment ya jijini Tanga kuja kufanya shoo Ijumaa oktoba 8 mwaka huu baada ya kukubaliana kulipwa ujira wa shilingi milioni 2.5.


Msanii huyo anatuhumiwa kuingia mitini na kushindwa kuhudhuria shoo hiyo kwa kile kinachodaiwa kuwa ni kutokana na kuachwa na ndege.


Kukosekana kwake kulisababisha vurugu kubwa katika ukumbi huo  kutoka kwa mashabiki waliokuwa wakitaka kurudishiwa pesa zao za kiingilio,ambapo katika vurugu hizo wacheza shoo wa msanii huyo na mwandaaji wa shoo hio walitiwa mbaroni na polisi .


Taarifa zaidi zimeeleza  kwamba msanii huyo alilipwa kiasi cha shilingi milioni 1.5 sanjari na kukatiwa  tiketi ya ndege ya kwenda na kurudi yenye thamani ya shilingi laki 3 unusu,ambapo aliwatanguliza wacheza shoo wake wanane jijini Arusha.


Kwa mujibu wa mkurugenzi wa kampuni ya  Arba,Mbwana Imamu, alisema kuwa Diamond alishindwa kutokea na hakuwa ametoa taarifa yoyote ya kutofika kwake kwenye shoo hiyo na kwamba muda wote walipokuwa wakiwasiliana  alikuwa akimwambia kuwa anakuja.


Ilipofika usiku wa manane  bila msanii huyo kutokea, mashabiki waliokuwa wametoa kiingilio wapatao 2000 ndani ya ukumbi huo walianza kuleta fujo wakishinikiza kurudishiwa fedha za kiingilio kiasi cha shilingi 10,000 kila mmoja  walizokuwa wamelipa.


Vurugu hizo ziliambatana na uvunjwaji wa viti, chupa, Glass, vioo  na samani mbalimbali za ndani na watu kupigwa wakiwemo ma-DJ waliokuwa wakichezesha muziki.


Hata hivyo polisi waliarifiwa na kufika katika eneo hilo ambapo walimtia mbaroni mwandaaji wa shoo hiyo pamoja na wacheza shoo wanne kati ya wanane wa Diamond ambao bado  wanashikiliwa katika kituo kikuu cha polisi mjini hapa, huku polisi ikimtaka msanii huyo kujisalimisha kituoni hapo.


Kwa mujibu wa mkurugenzi wa The blue Triple A, Papa King alisema kuwa hasara iliyopatikana kutokana na vurugu hizo ni shilingi milioni 3.5 na kwamba imetia doa ukumbi huo unaoheshimika hapa nchini na Afrika mashariki.


Nae mkurugenzi wa Arbab Mbwana Imamu alisema kuwa msanii huyo amemtia  hasara ya shilingi milioni 20 ambazo anamtaka kuzirudisha yakiwemo malipo ya uharibu wa ukumbi huo.


Diamond alipotafutwa kwa njia ya simu alisema kuwa hakufanya maksudi kutohudhuria shoo hiyo, bali aliachwa na ndege iliyopangwa iondoke majira ya saa 12 jioni katika uwanja wa ndege wa mwalimu Nyerere jana.


Hata hivyo alisema kuwa yupo tayari kufanya shoo yoyote  bure katika ukumbi huo ili kufidia hasara hiyo iliyotokea.


Kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Arusha, Afande Akili Mpwapwa alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa bado wanawashikilia wacheza shoo wanne wa Diamond kutokana na kosa la kusababisha  vurugu na auharibifu uliotokea katika ukumbi huo wa Triple A na Diamond anatakiwa kujisalimisha katika kituo hicho cha polisi jijini Arusha.

Categories: